Sunday, 15 December 2013

VAN PERSIE KUKOSA MECHI NANE

MANCHESTER United imepata pigo kubwa baada ya straika wake mahiri Robin van Persie kuumia paja na kwamba atakuwa nje ya uwanja kwa mwezi mmoja.
Fowadi huyo wa Uholanzi aliumia wakati akipiga kona iliyosababisha bao la Manchester United kwenye mechi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Shakhtar Donetsk Jumanne iliyopita na sasa majeraha hayo yatamweka nje ya uwanja hadi mwakani.
Majeraha hayo ni pigo kubwa kwa kocha David Moyes ambaye kwa sasa anahaha kuinusuru Manchester United kukwepa kipigo cha tatu mfululizo kwenye Ligi Kuu England wakati itakapomenyana na Aston Villa kesho Jumapili.
Van Persie atakosa mechi nane za mabingwa hao wa England ukianzia Aston Villa kesho Jumapili kwenye Uwanja wa Villa Park.
Moyes alisema: “Robin amepata majeraha ya paja na atakuwa nje kwa mwezi mmoja. Alikuwa anapiga kona dhidi ya Shakhtar na hapo alijiumiza paja. Tutamkosa tena Robin, safari hii kwa mwezi mzima.”
Mechi atakazikosa Van Persie ni dhidi ya Aston Villa, Stoke City, West Ham United, Hull City, Norwich City, Tottenham Hotspur na Swansea City mara mbili kwenye Ligi Kuu na Kombe la FA.

No comments:

Post a Comment