Tuesday, 10 December 2013

MCHUJO WA LOGARUSIC WAIVURUGA SIMBA SC

Kocha wa Simba, Zdravko Logarusic ameeleza kuwa kuna mambo mengi yanayotakiwa kufanyiwa kazi katika kikosi cha Simba ili timu ifanikiwe na jambo la kwanza aliloona halijakaa sawa ni mishahara ya wachezaji  


MCHUJO wa wachezaji wa Simba unaodaiwa kutangazwa na Kocha Zdravko Logarusic umezua zogo Simba kwani viongozi walitarajia kukutana naye haraka ili kufahamu vigezo vilivyotumika katika mchakato huo.
Inadaiwa Logarusic ametangaza wachezaji 26 wa kuendelea na Simba huku wengine sita wakitemwa kwa madai ya kutohitajika kikosini na kutakiwa kwenda kikosi B.
Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi ya Simba, Danny Manembe ameliambia Mwanaspoti kuwa hadi jana Jumatatu mchana majina hayo yalikuwa hayajafika mikononi mwao kwa kuyathibitisha kwani walipanga kufanya kikao na kocha huyo jioni ili kuyajadili.
“Hayo majina sijajua yametoka wapi maana kocha hawezi kuacha au kuwashusha wachezaji kutoka kikosi cha kwanza bila ya sisi watu wa ufundi kufahamu, tunakutana naye leo (jana Jumatatu) jioni na kuyapitia majina ya wachezaji anaodhani anataka kubaki nao kikosini au kuwatema.
“Tutatazama vigezo vilivyotumika na kama tukiridhishwa navyo tutapitisha maana mchezaji mwingine anaweza kukataa kucheza kwa mkopo au kwenda timu B kulingana na mkataba wake,” alisema Manembe.
Aliongeza: “Pia inawezekana kocha akaamua kuwapunguza aliowapunguza lakini akawa hayuko sahihi maana kuna wachezaji wametajwa kupunguzwa lakini hata mazoezini hawakufika hata mara moja, sasa labda tukutane naye tujue katumia vigezo gani kuwaacha.”
Baadhi ya wachezaji waliotajwa kuenguliwa kikosi cha kwanza ni Andrew Ntalla, Sino Augustino na Ibrahim Twaha ‘Messi’ Marceil Kapama, Rashid Ismail na Adeyun Seif.
Waliobaki ni Yaw Berko, Abuu Hashim, Omary Salum, Haruna Shamte, Issa Rashid, Said Nassor ‘Chollo’, Hassan Khatib, Joseph Owino, Miraji Adam, Gilbert Kaze, Said Ndemla, Jonas Mkude, Henry Joseph, William Lucian, Abdulhalim Humud, Ramadhan Singano, Ramadhan Chombo, Amri Kiemba, Uhuru Seleman, Haruna Chanongo, Amis Tambwe, Badru Ally, Edward Christopher, Awadhi Juma na Betram Mwombeki.
Kwa upande wake Sino aliiambia Mwanaspoti kuwa yupo tayari kwenda kucheza popote kwa mkopo kwani anaamini yanayotokea si maamuzi ya kocha.
“Kabla hata kocha hajafika niliambiwa na kiongozi mmoja kwamba, natakiwa kwenda kucheza kwa mkopo JKT Ruvu bila ya kufafanuliwa zaidi, sasa niliposikia haya nikaona ndiyo yale yale. Mimi ni mchezaji najiamini katika uwezo wangu na nitacheza popote pale.
“Mimi naamini kuna watu wameamua kumpa kocha majina haya na yaliandaliwa hata kabla hajafika.Wengine hawapo katika timu wameachwa, wengine wamebakizwa sasa kigezo kipi kimetumika,” alisema Sino.
Twaha ambaye anafahamika pia kama Messi, alisajiliwa Simba msimu huu akitokea Coastal Union alisema; “Mimi naumwa tangu Oktoba 10 nilipochanika nyama za paja, sasa naachwa kwa kigezo kipi? Labda kwa kuumwa, hata kama napelekwa kwa mkopo au timu B nitatumikia vipi?” Alihoji mchezaji huyo.



No comments:

Post a Comment