Tuesday, 17 December 2013

KASEJA ADAKA MASHUTI 17 YANGA

Kipa,Juma Kaseja.














KIPA,Juma Kaseja, juzi Jumamosi aliichezea Yanga mechi yake ya kwanza baada ya kurejea klabuni hapo hivi karibuni akitokea Simba na kudaka mashuti 17 katika dakika 90 za mchezo wa kirafiki dhidi ya KMKM ya Zanzibar. Mechi ilimalizika kwa Yanga kushinda mabao 3-2.
Kaseja ambaye aliwahi kuidakia Yanga kwa msimu mmoja 2009/2010, alirejea mwezi uliopita kwa mkataba wa miaka miwili baada ya kuachwa na Simba kabla ya kuanza msimu huu.
Mashabiki wa Yanga walipiga makofi ya kuashiria kumkubali Kaseja wakati timu zikiingia uwanjani naye aliwajibu kwa kuwanyooshea mikono.
Kaseja aligusa mpira kwa mara ya kwanza dakika ya sita baada ya kurudishiwa na beki wa kati, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, kisha akampasia Juma Abdul.
Katika kipindi cha kwanza Kaseja alidaka mashuti tisa yaliyoelekezwa langoni kwake na washambuliaji wa KMKM akina Ali Shiboli, Ibrahim Hamis na Haji Simba.
Hata hivyo, Kaseja alifungwa mabao mawili dakika za 69 na 72 wafungaji wakiwa ni Simba na Shiboli ambao walitumia vyema makosa ya mabeki wa Yanga waliojichanganya kuokoa hasa baada ya Cannavaro kutolewa dakika ya 65 na nafasi yake kuchukuliwa na Rajab Zahir.
Katika kipindi cha pili, Kaseja alidaka mashuti manane na kufanikiwa kupangua mipira miwili na kuifanya kuwa kona ambazo hazikuzaa matunda.
Mara baada ya mchezo huo, Kaseja aliliambia Mwanaspoti kwamba amefurahi kucheza mechi ya kwanza Yanga na kufanya vizuri licha ya kufungwa mabao mawili.
“Naona nimeanza vizuri na yaliyotokea ni mambo ya kimchezo tu, ninauamini ukuta wa Yanga na nadhani makosa yaliyojitokeza tutayarekebisha kwa kushirikiana na kocha,” alisema

No comments:

Post a Comment