Thursday, 26 December 2013

LUNYAMILA AANZA KUZUNGUMZA


Lunyamila akiwa amelala kitandani hospitalini .PICHA|MAKTABA 

HALI ya winga wa zamani wa Yanga na Taifa Stars, Edibily Lunyamila, inaendelea kuimarika baada ya kuanza kuzungumza kwa kifupi na watu wanaomtembelea kumjulia hali katika Hospitali ya Mwanyamala, Dar es Salaam, ambapo amelazwa.
Lunyamila alifikishwa hospitalini hapo Jumatatu ya wiki hii akitokea nyumbani kwake Mbezi Luis baada ya kuzidiwa alipopatwa na tatizo la kupumua. Hospitalini hapo alilazimika kufungiwa mitungi ya gesi ili kumsaidia kupumua.
Jana Jumatano asubuhi Mwanaspoti lilifika hospitalini hapo na kuweza kusalimiana na Lunyamila kwa kifupi kwani kutokana na ushauri wa madaktari, nyota huyo wa zamani haruhusiwi kuzungumza kwa muda mrefu.
“Nashukuru kidogo afadhali,” ndiyo kauli ya Lunyamila kwa mwandishi wa habari hizi aliyetaka kumjulia hali.
Ndugu wa Lunyamila anayemuuguza, Lameck John, alisema ripoti ya kwanza ya madaktari imesema winga huyo anasumbuliwa na homa ya matumbo, lakini amechukuliwa vipimo tena kutazama kama ana matatizo ya moyo.
“Wametuambia anaumwa homa ya matumbo lakini wanatazama pia kujua kama ana matatizo ya moyo,” alisema Lameck.
Juzi Jumanne, baadhi ya viongozi na wanachama wa Yanga walifika hospitalini hapo na kumhamisha mchezaji huyo kutoka wodi namba 5B na kumpeleka wodi namba 4 ambako anatibiwa katika mazingira mazuri zaidi.
Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Abdallah Bin Kleb, mjumbe wa Kamati ya Utendaji, Mohamed Bhinda na mchezaji wa zamani wa timu hiyo, Ali Mayayi, ndiyo walioratibu maboresho ya huduma anayopata Lunyamila hospitalini hapo.
Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi, naye ni miongoni mwa wadau wa michezo waliojitokeza kumfariji Lunyamila hospitalini hapo.
Wengine ni Juma Kaseja, Aboubakar Salum ‘Sure Boy’, Mohamed Hussein ‘Mmachinga’, Seleman Matola, Vincent Peter na Idd Moshi.

No comments:

Post a Comment