Tuesday, 17 December 2013

ARSENAL YAPEWA BAYERN MUNICH ULAYA

Wachezaji wa Bayern Munich wakishangilia 













ARSENAL imepewa kibarua kizito katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya hatua ya mtoano baada ya kupangwa kucheza na mabingwa watetezi, Bayern Munich, Februari mwakani.
Bayern inayofundishwa na Pepe Guardiola, kwa sasa imekuwa katika kiwango cha juu katika misimu mitatu iliyopita ambapo imefanikiwa kutinga fainali hizo mara mbili mfululizo na kutwaa ubingwa msimu uliopita katika pambano dhidi ya Borussia Dortmund lililofanyika mwezi Mei katika Uwanja wa Wembley.
Manchester City ambayo ni mara yao ya kwanza kufuzu hatua hiyo ya mtoano, imepewa mtihani mzito wa kukabiliana na Barcelona ambayo itaongozwa na mkali wao, Lionel Messi, ingawa kwa sasa ni majeruhi.
Manchester United ndio timu ya England iliyopata nafuu zaidi katika ratiba hii ya hatua ya mtoano na itapepetana na Olimpiakos ya Ugiriki katika pambano ambalo United inatazamiwa kupita.
Mshambuliaji wa kimataifa wa Ivory Coast, Didier Drogba, anatazamiwa kuwa kivutio katika pambano la mtoano kati ya Chelsea na Galatasaray baada ya ratiba kuwakutanisha vigogo hao wa London na Istanbul.
Cristiano Ronaldo ataiongoza Real Madrid kusafiri mpaka Ujerumani kukipiga na Schalke 04 wakati staa wa kimataifa wa Sweden, Zlatan Ibrahimovic, naye atafunga mkanda na timu yake PSG kwenda huko huko Ujerumani kuchuana na Bayer Leverkusen.
AC Milan baada ya kupita katika kundi lao wakishika nafasi ya pili nyuma ya Barcelona, nao wamepewa zawadi ya kwenda tena Hispania kukipiga na Atletico Madrid katika pambano linalotarajiwa kuwa kali na la kusisimua.
Wanafainali wa msimu uliopita, Borussia Dortmund wamepewa kibarua cha kwenda Ulaya Mashariki kukipiga na Zenit Petersburg ambayo inaongozwa na staa wa zamani wa Arsenal, Andrey Arshavin.
Timu zote zilizomaliza nafasi ya pili zitaanza kucheza mechi zake katika viwanja vya nyumbani na mechi za kwanza zitachezwa kati ya Februari 18/19 na Februari 25/26, wakati zile za marudiano zitachezwa kati ya Machi 11/12 na Machi 18/19.

Mwanasport.

No comments:

Post a Comment