Tuesday, 17 December 2013

SIMBA YAIZIMA KMKM, Logarusic apangua kikosi

Kikosi cha Simba.
 












SIMBA imeichapa KMKM ya Zanzibar mabao 3-1 katika mechi ya kirafiki iliyochezwa jana Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
Katika mechi hiyo ambayo ilikuwa ya kwanza kwa kocha mpya wa kikosi hicho, Zdravko Logarusic ambaye alianza kwa staili ya kuwahamisha namba baadhi ya wachezaji.
Kocha huyo raia wa Crotia alimpanga Issa Rashid ‘Baba Ubaya’ kucheza kama winga wa kushoto badala ya beki wa kushoto nafasi aliyokuwa akicheza siku zote na kumuanzisha Henry Joseph kama beki wa kati akicheza sambamba na Joseph Owino.
Henry alipangwa nafasi hiyo kutokana na uhaba wa mabeki wa kati baada ya Gilbert Kaze kuwa kwao Burundi akiwa mgonjwa wa kifua ingawa Simba tayari imemsajili beki mpya kutoka Gor Mahia ya Kenya Donald Musoti.
Katika mchezo huo ambao haukuhudhuriwa na mashabiki wengi, Logarusic pia alimuanzisha kipa wake mpya, Yaw Berko kwa mara ya kwanza huku timu hiyo ikitawala vyema kwenye safu ya kiungo ambayo iliongozwa na Jonas Mkude na Said Ndemla waliofunika katika nafasi hiyo.
Said Ndemla ndiye aliyeanza kuamsha shangwe kwa mashabiki wa Simba baada ya kufunga bao dakika ya 11 kwa shuti kali lililomshinda kipa wa KMKM, Mudathir Khamis kabla ya Edward Christopher kufunga la pili dakika ya 16.
Hata hivyo Simba walionekana kupwaya kipindi cha pili na kuwaruhusu KMKM kufunga bao la kwanza dakika ya 73 likifungwa na mchezaji wa zamani wa Simba, Alli Shiboli kwa penalti baada ya beki Omary Salum kumchezea rafu mshambuliaji huyo.
Hata hivyo wakati mashabiki wakidhani matokeo yatabaki hivyo Henry Joseph aliwainua tena mashabiki wa Simba vitini kwa kufunga bao la tatu kwa penalti dakika ya 88 baada ya Issa Abdallah kufanyiwa madhambi na beki Khamis Ally wa KMKM katika eneo la penalti.
Kikosi Simba: Berko, Haruna Shamte, Omary Salum, Henry Joseph, Joseph Owino,Jonas Mkude,Edward Christopher/William Lucian, Said Ndemla/Miraji Adam,Betram Mwombeki/Amiss Tambwe, Uhuru Seleman na Issa Rashid.

No comments:

Post a Comment